Thursday, December 22, 2011

Maaskofu, Mapadri washambuliwa

Na Edward Kinabo,

VIONGOZI wa dini wakiwemo baadhi ya maaskofu, mapadri na wachungaji wa madhehebu mbalimbali ya kikristu nchini, wameaswa kuacha tabia ya kuwatanguliza mbele wanasiasa katika kila shughuli ya kiroho wala kuzigeuza nyumba za ibada kuwa vijiwe vya kuwasafisha na kuwahalalisha watu wenye malengo binafsi ya kutafuta uongozi.

Tuhuma na ushauri dhidi ya viongozi wa dini nchini zilitolewa jana na Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa (Chadema), alipozungumza na waandishi wa habari mjini hapa, kutoa salaam zake maalum kwa viongozi wa dini kuelekea sikuu kuu za X mas na mwaka mpya wa 2012.

Msigwa alisema katika mwaka unaomalizika wa 2011 kulishamiri desturi ya baadhi ya wanasiasa hususan wale wa Chama cha Mapinduzi (CCM) kupenda kuwatumia vibaya baadhi ya viongozi wa dini na nyumba za ibada kama sabuni ya kujisafisha na ngazi ya kufikia malengo ya kuutafuta urais au ubunge na udiwani.

Alisema ingawa Kanisa ni mahali pa kusafishwa uchafu na kila mtu anakaribishwa, lakini pia si sahihi kwa kanisa au nyumba nyingine za ibada kutumika kusafisha watu kwa malengo yao ya kibinafsi.

“Ingawa kanisa ni mahali pa kusafishwa uchafu na kila mtu anakaribishwa, lakini tumkumbuke yule Simon Mchawi katika kitabu cha matendo ya mitume,aliyejaribu kununua kipawa cha Roho mtakatifu kwa faida yake binafsi, ndipo mtumishi wa Mungu Petro alipomwambia apotelee mbali pamoja na pesa yake”, alisema Mchungaji Msigwa.

Aliwataka viongozi wa dini wenzake wasikubali kamwe kuwa mawakala wa kufanikisha kile alichokiita “mbio za urais mchafu”, wala kuwa chini ya wanasiasa, kwani jukumu la viongozi wa dini kwa binadamu ni zito na kubwa kuliko uroho wa madaraka aliodai kuwa ndio unaowakimbiza baadhi ya wanasiasa kwenye nyumba za ibada.

“Kanisa likitakiwa kuzinduliwa, mwanasiasa, uzinduzi wa nyimbo ya injili, mwanasiasa, ununuzi wa magitaa, mwanasiasa, ununuzi wa maspika, mwanasiasa. Hivi hawa wanasiasa wana upako gani kana kwamba kazi ya Mungu haiwezi kufanyika bila wao?

Sisi viongozi wa dini tunapaswa kuwa viongozi na sio wafuasi wa wanasiasa, tunapaswa kuwaonyesha njia wanadamu wote wakiwemo wanasiasa na sio wanasiasa watuonyeshe njia sisi, maana kufanya hivyo ni kulishusha thamani neno la Mungu”, alisema

Ingawa hakuwataja kwa majina baadhi ya wanasiasa wa CCM aliodai wanakimbilia makanisani kutafuta madaraka, lakini Edward Lowassa (Mbunge wa Monduli), Samuel Sitta (Waziri Afrika Mashariki) na Bernard Membe (Waziri Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa), ndio wamekuwa wakionekana zaidi kwenye matukio ya kanisa huku matukio hayo yakihusishwa na mbio za urais 2015.

“Ni udhalilishaji mkubwa wa huduma ya kiroho pale sisi viongozi wa dini tunapowatanguliza wanasiasa kwenye kila shughuli kama ya uzinduzi wa makanisa au albamu za nyimbo za kidini, kana kwamba wanasiasa ndio wenye upako, utukufu na mamlaka zaidi ya kubariki kinachozinduliwa kuliko sisi viongozi wa dini wenyewe.

“Tusikubali nyumba takatifu za ibada zigeuzwe viwanja vya kampeni za kisiasa na wala tusiwe chanzo cha kuiingiza nchi yetu katika mgawanyiko na machafuko ya kidini kwasababu tu ya kuwabeba baadhi ya wanasiasa ambao ama kwa sababu ya uchafu wao au umma kukosa imani nao, wameona hawawezi tena kuwa na uhalali wa kujitangaza wala kujijenga tena kwenye majukwaa ya kisiasa bila kwanza kukimbilia makanisani”, alisema Mbunge huyo na kuongeza:

“Binafsi naamini, mwanasiasa msafi anayejiamini na anayemcha Mungu kwelikweli haitaji harambee au tukio lolote la kujinadi kanisani , maana huko si pahali pake”

Alisema anafahamu kuwa taifa kwa ujumla wake lina hali duni kimaisha zinazowagusa pia viongozi wa kiroho, lakini hali hiyo isiwafanye baadhi ya viongozi wa dini kusahau misingi yao ya kitume kana kwamba Mungu aliyewaita amewaacha.

“Tunapokwenda kusherehekea siku kuu hii ya X Mas na Mwaka Mpya, ninawasihi tena viongozi wenzangu wa kidini, kwamba tumkumbuke mtumishi wa nabii Elisha, aliyeitwa Gehazi, ambaye alipenda pesa na zawadi akasahau mwito wake wa kitume mpaka ukoma wa Nahaman ukahamia mwilini mwake.

Na tumkumbuke Yuda Eskarioti ambaye alimuuza mwokozi wetu, Yesu Kiristu, kwa vipande thelathini vya fedha, na kwa hiyo, sisi viongozi wa dini tusikubali kamwe kuwauza Watanzania wenzetu kwa pesa za wanasiasa wachafu”, alisema mbunge huyo ambaye pia ni mchungaji wa kanisa la Vineyard.

Alisema anamini kuwa viongozi wa dini wakisimama imara bila kuyumba, Tanzania inayougua umaskini, ujinga, maradhi na ufisadi, hatimaye itaponywa.

Mwisho.

Waraka wa Msigwa kwa viongozi wa dini Tanzania: Kuweni macho na wanasiasa hawa...

Kwa nafasi yangu kama raia, Mbunge ninayewakilisha wananchi wa Jimbo la Iringa Mjini na Watanzania wote kwa ujumla na mmoja wa viongozi wa dini/dhehebu nchini, naomba kutumia fursa yenu na ya vyombo vyenu vya habari kutoa ujumbe mahsusi kwa viongozi wenzangu wa kidini kwa manufaa ya taifa letu.

Ninapowasilisha salaam zangu hizi za X-Mas na Mwaka mpya wa 2012, ningependa kusisitiza yafuatayo kwa viongozi wenzangu wa dini, kuhusiana na nini hasa unapaswa kuwa wajibu wetu kuhusiana na mwenendo wa viongozi wetu wa kisiasa (mimi pia nikiwa mmoja wao);

1. Nianze kwa, kuwapongeza viongozi wenzangu wote wa dini waliojitokeza hadharani au kupitia vyombo vya habari hivi karibuni kupinga kusudio au mpango wa kuongeza posho za vikao kwa wabunge. Suala hili limegusa hisia za Watanzania wengi wakiwemo viongozi wenzangu wa dini ambao nami naungana nao kuzipinga nikisisitiza msimamo wa siku nyingi wa chama chetu (Chadema).

2. Pongezi hizi zinazingatia ukweli kuwa katika suala hili la posho,Baadhi ya viongozi wa dini wameweza kuchukua wajibu wao kikamilifu wa kuwa juu ya wanasiasa wenye malengo mabaya tofauti na desturi iliyoanza kujengeka hivi karibuni ya baadhi ya wanasiasa hususan wale wa Chama cha Mapinduzi (CCM) kupenda kuwatumia vibaya baadhi ya viongozi wa dini na nyumba za ibada kama sabuni ya kujisafishia uchafu wao na ngazi ya kufikia malengo ya kuutafuta urais au ubunge na udiwani (uongozi mchafu). Ingawa kanisa ni mahali pa kusafishwa uchafu na kila mtu anakaribishwa, lakini tumkumbuke yule Simon Mchawi katika kitabu cha matendo ya mitume,aliyejaribu kununua kipawa cha Roho mtakatifu kwa faida yake binafsi, ndipo mtumishi wa Mungu Petro alipomwambia apotelee mbali pamoja na pesa yake.

3. Nawasihi viongozi wa dini wenzangu kwamba kamwe tusikubali kuwa mawakala wa kufanikisha mbio za urais mchafu. Tusikubali kuwa chini ya wanasiasa maana jukumu letu la kuwanusuru wanadamu kiroho kwa kuwaongoza kumcha Mungu, ni jukumu zito na kubwa kuliko uroho wa madaraka unaowakimbiza baadhi ya wanasiasa kwenye nyumba za ibada.

4. Ni udhalilishaji mkubwa wa huduma ya kiroho pale viongozi wa dini tunapowakaribisha wanasiasa kufanya shughuli kama za uzinduzi wa makanisa au albamu za nyimbo za kidini kana kwamba wao ndio wenye upako, utukufu na mamlaka zaidi ya kubariki kinachozinduliwa kuliko sisi viongozi wa dini wenyewe.

5. Tabia kama hii ya kuwatanguliza mbele wanasiasa kwenye shughuli za kiroho badala ya kuacha huduma hii ijitegemee yenyewe (maana Mungu ni Mkuu na mwenye uwezo kuliko siasa), kwa namna moja au nyingine imekuwa ndio kichocheo cha kufanya wanasiasa kutafuta pesa kwa gharama yoyote, ilimradi wakiitwa kwenye mialiko hiyo waweze kutoa fungu kubwa wakiamini itawajenga kisiasa hata kama hawana nia ya kweli na Mungu.

6. Tusikubali kamwe kutumiwa vibaya na wanasiasa wanaojipenyeza kwenye matukio mbalimbali kama ya harambee na uzinduzi wa albamu za nyimbo za kiinjili, kwa lengo la kujitangaza, kujisafisha na kujipendekeza kwa umma uliowakataa au kukosa imani nao.

7. Tusikubali nyumba takatifu za ibada zigeuzwe viwanja vya kampeni za kisiasa na wala tusiwe chanzo cha kuiingiza nchi yetu katika mgawanyiko na machafuko ya kidini kwasababu tu ya kuwabeba baadhi ya wanasiasa ambao ama kwa sababu ya uchafu wao au umma kukosa imani nao, wameona hawawezi tena kuwa na uhalali wa kujitangaza wala kujijenga tena kwenye majukwaa ya kisiasa bila kwanza kukimbilia makanisani. Binafsi naamini, mwanasiasa msafi anayejiamini na anayemcha Mungu kwelikweli haitaji harambee au tukio lolote la kujinadi kanisani , maana huko si pahali pake.

8. Najua kuwa Watanzania wengi wanakerwa na tabia ya baadhi ya sisi viongozi wa dini kama maaskofu, wachungaji na mapadri kubabaikia wanasiasa kwa kiasi cha kuonekana wanaidhalilisha huduma hii kuu. Kanisa likitakiwa kuzinduliwa – mwanasiasa, uzinduzi wa nyimbo ya injili – mwanasiasa, ununuzi wa magitaa – mwanasiasa, ununuzi wa maspika – mwanasiasa. Hivi hawa wanasiasa wana upako gani kana kwamba kazi ya Mungu haiwezi kufanyika bila wao?

9. Tunapokwenda kusherehekea siku kuu hii ya X Mas na Mwaka Mpya, ninawasihi tena viongozi wenzangu wa kidini, kwamba tumkumbuke nabii Baalam ambaye vitabu vitakatifu vinaeleza jinsi alivyoifanyia biashara huduma yake ya kinabii mpaka alisababisha Punda aongee;

Tumkumbuke mtumishi wa nabii Elisha, aliyeitwa Gehazi, ambaye vitabu vitakatifu vinatufundisha kwamba alipenda pesa na zawadi akasahau mwito wake wa kitume mpaka ukoma wa Nahaman ukahamia mwilini mwake;

Tumkumbuke Esau aliyeuza haki ya uzaliwa wake wa kwanza kwa njaa ya muda mfupi (dengu,mlo moja tu);

Na tumkumbuke Yuda Eskarioti ambaye alimuuza mwokozi wetu, Yesu Kiristu, kwa vipande thelathini vya fedha, na kwa hiyo, sisi viongozi wa dini tusikubali kamwe kuwauza Watanzania wenzetu kwa pesa za wanasiasa wachafu.

10. Nasisitiza tena, kwamba sisi viongozi wa dini tunapaswa kuwa viongozi na sio wafuasi wa wanasiasa, tunapaswa kuwaonyesha njia wanadamu wote wakiwemo wanasiasa na sio wanasiasa watuonyeshe njia sisi, maana kufanya hivyo ni kulishusha thamani neno la Mungu.

11. Naamini kama taifa kwa ujumla tuna hali za duni za kimaisha zinazotugusa pia sisi viongozi wa kiroho, lakini hii isisababishe tukasahau misingi yetu ya kitume kana kwamba Mungu aliyetuita ametuacha. Naamini sisi viongozi wa dini tukisimama imara bila kuyumba, Tanzania yetu inayougua umaskini, ujinga, maradhi na ufisadi, hatimaye itaponywa. Hizi ndio salamu zangu za mwaka mpya kwa viongozi wa dini ambao naamini kupitia wao Watanzania wote wataongozwa vema

Nawatakia kheri na fanaka ya X- Mas na Mwaka Mpya.
Mungu ibariki Tanzania.

Mchungaji Peter Msigwa
Mbunge Jimbo la Iringa Mjini

Tuesday, December 20, 2011

Katiba Mpya yayeyuka

Na Edward Kinabo

NDOTO ya Watanzania kupata katiba mpya imetoweka baada ya serikali ya rais Jakaya Kikwete kuamua kuunda tume ya kukusanya maoni ya katiba kabla ya kurekebisha sheria inayolalamikiwa, Tanzania Daima Jumatano limebaini.

Waziri wa Sheria na Katiba, Celina Kombani, amethibitisha wiki hii kwamba Serikali haina nia ya kuifanyia marekebisho Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2011 na kwamba kinachosubiriwa hivi sasa ni Mkuu huyo wa nchi kuunda tume ya mabadiliko ya katiba kwaajili ya kukusanya maoni.

Kombani akihojiwa kwenye mahafali ya Chuo cha Taaluma ya Habari jijini Dar es Salaam (DSJ), alisema sheria hiyo ni lazima tume hiyo iundwe kwanza kabla ya marekebisho yoyote kufanywa.

Msimamo huo unaonekana dhahiri kwenda kinyume na kile alichokubali Kikwete kwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), walipokutana naye Ikulu jijini Dar es Salaam hivi karibuni, kwamba ipo haja ya sheria hiyo kufanyiwa marekebisho kabla ya kuanza kutumika.

Msimamo huo mpya unamaanisha kuwa tume hiyo itaundwa na wajumbe wa kuteuliwa na Rais chini ya utaratibu uliowekwa na sheria iliyosainiwa, jambo ambalo limekuwa likipingwa na wadau wengi.

Wanaopinga utaratibu huo wamekuwa wakisisitiza kuwa, “wajumbe wa tume wakiteuliwa na Rais hawatakuwa huru na watalazimika kulipa fadhila kwa Rais atakayewateua na chama chake (CCM)”

Wanasema utaratibu wa sheria hiyo ukitumika ni dhahiri kuwa tume itafanya kazi ya kuchakachua maoni muhimu ya wananchi na kuhakikisha inadumisha yote yanayotakiwa na CCM hata kama yatakuwa kinyume na matakwa ya wengi.

Wanatoa mfano kuwa wakati wananchi wengi wanaoonekana kukerwa na muungano wa serikali mbili na kutaka katiba mpya iruhusu muundo wa Serikali tatu, sera ya CCM siku zote imekuwa ni kudumisha serikali mbili.

Aidha, baadhi ya wadadisi wa masuala ya kisiasa wamelieleza Tanzania Daima Jumatano kuwa CCM haijawahi hata siku moja kuwa na ajenda ya kutaka katiba mpya.

Kwamba inachofanya sasa ni kujaribu tu kuwatuliza wananchi kwa kuwapa matumaini hewa kuwa katiba mpya inakuja, wakati wamepitisha sheria inayowawezesha kuutawala mchakato mzima na kuamua aina ya katiba waitakayo kwa maslahi yao ya kichama na kiserikali.

“CCM siku zote wamekuwa wakiipigania katiba ya sasa ibaki. Kama tutazubaa na kuacha sheria hii bila marekebisho, hakuna katiba mpya itakayotokea… maana tume itakuwa ni yao na vyombo vyote vya kuamua katiba kama bunge la katiba, mabaraza ya katiba na kura za maoni, vitatawaliwa nao”, ameeleza Jaji mmoja mstaafu kwa sharti la kutotajwa jina lake.

Chadema kupitia Waraka wao kwa Kikwete, walipendekeza badala ya wajumbe wa tume kuteuliwa na Rais pekee, sheria irekebishwe kuruhusu wajumbe kupatikana kwa kuchaguliwa kutoka kwenye taasisi za kiraia, kidini, kitaaluma, vyama vya siasa na wachache kuteuliwa na Rais, ili kuwa na tume huru na yenye uwakilishi mpana wa kulinda maslahi ya umma katika mchakato mzima wa katiba mpya.

Ili kuondoa uwezekano wa upande mmoja wa muungano kuingilia mambo yasiyo ya muungano na kuamua muelekeo wa kikatiba wa upande wa pili, chama hicho kikuu cha upinzani pia kilipendekeza kwa Rais kwamba kuundwe tume mbili za katiba, moja itakayokusanya na kuratibu maoni ya wananchi kuhusu katiba mpya kwa ajili ya masuala yasiyokuwa ya Muungano ya Tanganyika, na ya pili itakayokusanya na kuratibu maoni ya wananchi juu ya masuala ya Muungano.

Mbali na Chadema, makundi ya kijamii na asasi nyingi zimekuwa zikipinga tume ya katiba kuundwa na Rais na kutaka sheria nzima ifanyiwe marekebisho makubwa.

Baadhi ya makundi hayo ni pamoja na Chama cha Mawakili Tanganyika, Chama cha Majaji Wastaafu, Chama cha Wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na asasi zaidi ya180 zinazounda Jukwaa la Katiba.

Wengine ni Umoja wa Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), Umoja wa Madhehebu ya Kidini Tanzania (Inter-Religion Council for Peace in Tanzania (IRCPT) na watu mashuhuri kama Jaji Mkuu mstaafu, Barnabas Samatta na msomi mashuhuri nchini, Profesa Issa Shivji wamedaikatika mijadala inayoendelea nchi nzima

Mwisho.

Friday, December 2, 2011

Ushindi wa JK wazidi kutia shaka

Na Edward Kinabo

UHALALI wa Rais Jakaya Kikwete kuwa madarakani unazidi kutia shaka baada ya ripoti ya mwisho ya waangalizi wa Umoja wa Ulaya kutoa maelezo yanayothibitisha kuwapo kwa mwanya mkubwa wa kura kuibiwa na matokeo kubadilishwa katika uchaguzi mkuu wa Rais uliofanyika mwaka jana (2010).

Wakati Rais Kikwete na chama chake walidai kura zisingeibiwa kwa sababu kila chama huruhusiwa kuweka wakala wake, ripoti hiyo ya ujumbe wa waangalizi wa uchaguzi mkuu kutoka Jumuiya ya Ulaya (EU) inawaumbua, baada ya kueleza waziwazi bila kumung’unya maneno kwamba mawakala wa vyama vya siasa na waangalizi wa uchaguzi hawakuruhusiwa kushuhudia ujumlishaji wa matokeo ya uchaguzi wa rais.

Ujumbe wa waangalizi hao wa EU ukiongozwa na Mbunge wa Bunge la Ulaya, David Martin, ulikuwepo nchini tangu Septemba 29 hadi Novemba 28 mwaka jana na ulisambaza waangalizi wake 103 katika mikoa yote 26 ya Bara na Visiwani.

Katika ripoti hiyo ambayo Tanzania Daima Jumapili inayo nakala yake, wataalamu hao wameeleza kuwa matokeo ya kura za urais mwishowe yalijumlishwa na viongozi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) wakiwa peke yao bila kushuhudiwa na mawakala wa vyama vya siasa, utaratibu ambao kwa mtazamo wa kawaida, ulitoa mwanya mkubwa kwa kura kuibiwa au matokeo halali kubadilishwa, huku ukiwepo uwezekano wa Kikwete kupendelewa kwa sababu ya kile kinachofahamika kuwa ndiye aliyewateua kuiongoza tume hiyo kwa mamlaka yake ya uteuzi kama rais.

“Matokeo ya uchaguzi wa rais wa Jamhuri ya Muungano yalijumlishwa na makamishna wa NEC. Matokeo ya kila jimbo la uchaguzi yalitumwa Idara ya Teknolojia ya Habari ya NEC (NEC IT Department) kwa njia ya kompyuta, ambapo yalipokewa na makamishna wa NEC.

Mawakala wa vyama vya siasa na waangalizi wa uchaguzi hawakuruhusiwa kufuatilia ujumuishaji wa matokeo ya uchaguzi wa rais”, ilisema ripoti hiyo yenye kurasa 61.

Wakizidi kuonyesha jinsi ujumlishaji wa kura za urais ulivyogubikwa na usiri mkubwa uliokuwa na nia mbaya, wataalamu hao katika ukurasa wa 51 wa ripoti yao, wanasema:

“Licha ya kuwapo hakikisho la waangalizi wa uchaguzi kuruhusiwa kuwepo kwenye hatua zote za uchaguzi, ujumbe wa Waangalizi wa Uchaguzi wa Jumuiya ya Ulaya (EU EOM) haukuruhusiwa kuwepo kwenye hatua muhimu za michakato ya ujumlishaji na uthibitishaji wa matokeo, hususan matokeo ya uchaguzi wa rais.”

Wakizungumzia zaidi mfumo wa usiri uliotumika kujumlisha matokeo na ulivyoweza kuathiri uhalali wa matokeo yenyewe, waangalizi hao wamesema: “Taratibu za kuhesabu na kujumlisha matokeo katika ngazi ya kituo cha kupigia kura; wilaya na taifa maelezo yake ingefaa yatolewe wazi moja kwa moja kwenye kifaa ambacho yanaweza kurekodiwa na kuonyeshwa, kisha kuonekana wazi kwa macho kwa wadau wote. Kufanya hivyo, kungedumisha uhalali wa matokeo na uwazi wa tume ya uchaguzi”.

Ikigusia mwenendo wa kampeni na matumizi ya rasilimali za serikali, ripoti hiyo imeonyesha jinsi vyombo vya habari vya serikali vilivyoripoti zaidi kampeni za CCM na chama hicho kunufaika na muundo wa kiutawala kuliko vyama vya upinzani, huku ikibainisha kuwa vyama vya upinzani havikukata tamaa ya kushindana kutokana na hali hiyo.

“Chama kikuu cha upinzani cha CHADEMA upande wa Bara, taratibu kilizidi kuungwa mkono baada ya kipindi kirefu cha kampeni,” ripoti hiyo inasema.

Pia wachunguzi hao wanasema kutokana na kuwepo kwa dosari nyingi kwenye mchakato wa kujumlisha matokeo ya uchaguzi wa rais kwenye baadhi ya majimbo, Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kiliandikisha lalamiko NEC Novemba 4, mwaka jana na kuitaka isitishe kutangaza matokeo na badala yake irudie upya uchaguzi, lalamiko ambalo hata hivyo lilitupiliwa mbali na NEC, ambayo ilidai kuwa tuhuma zilizotolewa zingepaswa kuwasilishwa kwa wasimamizi wa kura.

Katika ukurasa wa 55 wa ripoti hiyo, waangalizi hao wamependekeza kuanzishwa kwa haki ya matokeo ya uchaguzi wa rais kupingwa mahakamani.

Kwa upande mwingine ripoti hiyo imeeleza kile kinachoonekana kuwa ni busara na hekima aliyoonyesha Dk. Slaa kwa kukataa kutoa mwito kwa wananchi kufanya vurugu baada ya kutoridhishwa na matokeo ya urais.

“Dk. Slaa hakutoa mwito wowote wa kufanya vurugu au kuuchochea mjibizano ulioratibiwa na wafuasi wa chama chake, bali alitaka kuwe na uchaguzi mpya wa urais wa Jamhuri ya Muungano kwa manufaa na faida ya taifa zima kutokana na matokeo ya uchaguzi yaliyotolewa na NEC kutodhihirisha matakwa ya wapiga kura,” ilifafanua zaidi ripoti hiyo.

Gazeti hili liliwahi kuandika taarifa nyingine za uchunguzi zilizokuwa pia kwenye mitandao ya kompyuta (internet) zilizoeleza kuwa Dk. Willibrod Slaa aliyekuwa mgombea urais kupitia CHADEMA alishinda uchaguzi huo kwa kupata asilimia 64 ya kura zilizopigwa.

Taarifa hizo zilieleza kuwa matokeo zaidi ya urais yalichakachuliwa katika majumlisho ya mwisho ya kura nchi nzima, ambapo NEC inadaiwa ilipunguza kura za Dk. Slaa hata zile zilizokuwa zimeshuhudiwa kwa pamoja na mawakala wa vyama vya upinzani katika ngazi za majimbo.

Hata hivyo kama ilivyotarajiwa, Mwenyekiti wa NEC, Jaji Lewis Makame, alikanusha vikali taarifa za Dk. Slaa kushinda urais kupitia gazeti la Uhuru linalomilikiwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Waraka wa Kinabo: Kuna umuhimu gani Wapinzani kuungana?

WATANZANIA wenzangu, kama nilivyosema katika waraka wangu kwenu wiki mbili zilizopita, ukombozi wa taifa letu dhidi ya umaskini, ujinga, maradhi na ufisadi, hauwezi kupatikana chini ya utawala wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kilichoshindwa kufanya hivyo katika kipindi cha miaka 47 ya utawala wake.

Nilieleza kuwa CCM imeshathibitisha kupitia viongozi wake, makada, na utendaji wa serikali yake kuwa ni chama ambacho hakina dhamira ya dhati ya kusimamia uwajibikaji na adilifu kwa ajili ya maendeleo ya watu.

Maendeleo yaliyopatikana chini ya utawala wa chama hiki hayalingani na umri wa uhuru wetu wala utajiri wa rasilimali za nchi yetu. Aidha, hayalingani na wito wa wananchi katika kulipa kodi na kutoa michango ya kusaidia miradi ya maendeleo.

Mafanikio kidogo ambayo CCM imekuwa ikiyaita kuwa ni maendeleo na kuyatumia katika kila uchaguzi kulaghai wananchi, kwa kiasi kikubwa yanalingana na ufisadi uliokithiri nchini.

Wingi wa ufisadi ndio udogo wa maendeleo yetu! Katika kipindi hiki ambacho taifa letu linakabiliwa na matatizo makubwa ya kukithiri kwa ufisadi na kuongezeka kwa makali ya maisha, wajibu wetu mkuu unapaswa kuwa ni kutafakari njia mbadala ya kutufikisha kwenye ukombozi tunaouhitaji na kuifuata njia hiyo.

Mfumo wa siasa ya vyama vingi nchini ndiyo fursa ya kwanza tunayopaswa kuitumia. Uwepo wa vyama vya upinzani unatupa fursa ya kutafuta itikadi, sera, mipango na mikakati ya kutekeleza yale tunayoyahitaji. Tunahitaji kasi, ufanisi na uwajibikaji unaozidi ule ulioonyeshwa na CCM kwa kipindi cha miaka 47 sasa.

Hata hivyo, nguvu ya CCM siku zote imekuwa ikijenga hofu kwa jamii kuwa ni vigumu kwa chama chochote cha upinzani kuweza kuing’oa CCM madarakani.

Kwa sababu hii, imekuwa ikipendekezwa na kusisitizwa kwa muda mrefu kwamba, ili kuiondoa CCM madarakani, vyama vya upinzani nchini ni lazima vishirikiane na kusimamisha mgombea mmoja katika kiti cha urais, viti vya ubunge, udiwani na katika viti vya chaguzi za serikali za mitaa.

Leo waraka wangu kwenu unahusu mtazamo na imani hii kubwa iliyojengwa kwa wananchi, nawasihi tujiulize maswali haya: “Kuna umuhimu gani kwetu, wapinzani wakishirikiana ili kuing’oa CCM? Hivi ni kweli kuwa CCM haiwezi kung’olewa hadi vyama vya upinzani viungane au vishirikiane? Tutafakari pamoja.

Wahenga wetu waliowahi kuishi karne nyingi nyuma, walituusia kuwa umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu. Hata hivyo katika medani za siasa za sasa, nikizingatia uzoefu wa ushirikiano wa vyama vya siasa nchini na ule wa nchi jirani ya Kenya, nasita kukubaliana moja kwa moja na dhana ya vyama vya upinzani kuwa katika ubia wa kisiasa.

Muungano au ushirikiano wa vyama vya siasa ni jambo lenye mantiki lakini katika mfumo wa vyama vingi umoja wa vyama vya upinzani unaweza usiwe na tija kwa wananchi.

Ikiwa vyama vitakuwa kwenye ushirikiano au muungano wa kisiasa kwa lengo tu la kukitoa chama tawala madarakani, bila kujipanga jinsi watakavyoweza kuunda serikali na kuwaondolea wananchi umaskini na matatizo mengine yanayowakabili, muungano au ushirikiano huo unaweza kuwa ni wa madhara makubwa kwa taifa.

Hata kama CCM ni tatizo bado ushirikiano wowote wa vyama vya wapinzani wenye lengo tu la kuing’oa CCM madarakani hauwezi kuwa na manufaa kwa taifa. Kuiondoa CCM madarakani ni jambo moja na kuiletea Tanzania maendeleo ni jambo jingine.

Baadhi ya watu wamekuwa wazito kutofautisha mambo haya mawili ambayo yanapaswa kwenda pamoja. Lazima malengo yawe zaidi ya kuiondoa CCM madarakani, vinginevyo ushirikiano wa vyama vya upinzani dhidi ya chama kinachotawala hauwezi kuwa na mantiki wala manufaa kwa Watanzania.

Kwa mfano katika ushirikiano wa kisiasa unaoyumba au uliovunjika kati ya vyama vikuu vinne vya upinzani, Chadema, CUF, TLP na NCCRMageuzi, vyama hivi kila kimoja kina itikadi, sera na mtazamo tofauti kuhusu jinsi kitakavyoongoza nchi iwapo kitapata ridhaa hiyo kutoka kwa wananchi.

CUF inajitambulisha kama chama cha itikadi ya Kileberali, Chadema inafuata itikadi ya mrengo wa kati, na NCCR wana mguso wa kijamaa.

Ikiwa vyama hivi vitaendelea kushirikiana kwa lengo la kusimamisha mgombea mmoja ili kuitoa CCM madarakani, serikali itakayoundwa na vyama hivi itafuata sera zipi? Wenzetu wanaotaka vyama hivi vishirikiane au viungane wakiamini kuwa kwa kufanya hivyo CCM itang’olewa, hivi wameainisha uwiano wa sera na misimamo ya vyama hivi kabla ya kuvitaka viendelee kufanya hivyo? Binafsi, naamini kuwa tunapaswa kuamka zaidi na kuimarisha mazingira ya kidemokrasia badala ya kushikilia hoja ya vyama kuungana.

Sioni haja ya kuilazimisha jamii kuchagua rangi nyeusi na nyeupe tu, kama jamii tunapaswa kutambua kuwa kuna nyekundu, bluu na kahawia pia. Tuondoe dhana ya uwili, CCM na upinzani, ndiyo na hapana, ukweli na uongo! Dhana ya uwili ina tofauti ndogo sana na mfumo wa chama kimoja tuliokwisha kuuacha.

Kunatakiwa kuwepo ushindani wa fikra, hoja nzito na sera mbadala. Tusitengeneze NARC nyingine Tanzania, kama ile ya Kenya ambayo malengo yake yalikuwa kuiondoa KANU pekee.

Vyama viungane kama malengo, maono au itikadi zao zinawiana na si kwa lengo la kuing’oa CCM tu. Ushirikiano au muungano usio makini wa vyama vya upinzani vyenyewe, au chama tawala na vyama vya upinzani, unaweza kusababisha kuundwa kwa serikali kubwa sana pindi muungano huo unaposhinda uchaguzi.

Ukweli ni kwamba, sisi ni binadamu, hisia za uchama zitaendelea kuwepo hata baada ya chama kimoja kuundwa, watu wataangalia waliokuwa CUF wapewe majimbo mangapi kugombea, Chadema, TLP na kadhalika.

Iwapo muungano utashinda ipo hatari ya kuundwa serikali kubwa kwa minajili ya kuridhisha kila chama kilicho kwenye muungano au ushirikiano huo (iwapo sheria ya vyama vya siasa itarekebishwa.

Muungano unaweza kupata shinikizo la kuridhisha kila chama kilicho kwenye muungano husika kitoe viongozi wa kuunda serikali. Hapa ndipo tunapoweza kuwa na wizara moja yenye mawaziri zaidi ya watatu na matokeo yake ni kuwa na bajeti kubwa mno kwa ajili ya kugharamia shughuli za utawala serikalini kuliko miradi ya maendeleo kwa ajili ya wananchi.

Kwa hiyo ushirikiano wa vyama vya upinzani wenye lengo tu la kuing’oa CCM hauwezi kuwa na manufaa kwetu. Kwa sababu hii kuyumba au kuvunjika kwa ushirikiano wa Chadema, CUF, TLP na NCCRMageuzi hakuwezi kuwa na madhara yoyote ya msingi kwetu sisi wananchi.

Bila shaka kuyumba au kuvunjika kwa ushirikiano wa vyama hivi kutatupa fursa nzuri zaidi chama au vyama vyenye sera nzuri na dhamira ya dhati ya kuziba pengo la upungufu wa CCM.

Hivi ni kweli kuwa CCM haiwezi kung’olewa hadi vyama vya upinzani viungane au viwe katika ushirikiano wa kisiasa? Msingi wa swali hili ni kuwa wapo wanaoamini kuwa sababu kuu ya vyama vya upinzani kushindwa katika chaguzi zilizopita ni kutosimamisha mgombea mmoja.

Kwamba vimekuwa vikigawana kura na kuiacha CCM ikishinda. Kwamba ili vyama vya upinzani viweze kuishinda CCM ni lazima viungane au vishirikiane, vinginevyo CCM itatawala milele. Binafsi siamini hivyo, sikubaliani na ulazima huo.

Naamini kuwa chama kimoja cha siasa chenye dhamira ya kweli, sera nzuri na mikakati mizuri na endelevu ya kufanya siasa na inayoweza kuwaridhisha wananchi kuwa itawakomboa, kinaweza kuishinda CCM.

Chama chochote kinachoweza kuthibitisha uwezo na dhamira yake ya kuwatumikia wananchi kuanzia bungeni kinaweza kuaminiwa na umma na kupata ridhaa ya kuongoza dola chenyewe bila kulazimika kuungana na vyama vingine.

Uzoefu wa uchaguzi mkuu uliopita uliompa Rais Kikwete ushindi mkubwa wa zaidi ya asilimia 80 unaweza kuthibitisha imani yangu. Miongoni mwa vyama vilivyoshiriki kwenye uchaguzi ule katika kiti cha urais ni CCM, Chadema, CUF, TLP, NCCR-Mageuzi, PPT Maendeleo, Demokrasia Makini, DP na SAU.

Mgombea wa urais wa CCM katika uchaguzi ule, Jakaya Mrisho Kikwete alipata ushindi wa zaidi ya asilimia 80, maana yake ni kwamba tukichukua kura za vyama vya upinzani zaidi ya nane vilivyosimamisha wagombea wake bado zisingeweza kutosha kuzidi kura za mgombea wa CCM.

Vyama vyote vya upinzani vilivyoshiriki kwenye uchaguzi ule kiti cha urais vilipata si zaidi ya asilimia 19 ya kura, wakati Kikwete wa CCM alipata zaidi ya asilimia 80. Kwa manti hii hoja kwamba vyama vya upinzani hushindwa kwa sababu ya kugawana kura haina mashiko.

Hushindwa kwa sababu ya udhaifu wao na sababu nyingine zilizo nje ya udhaifu wao, likiwemo tatizo la mfumo wetu wa uchaguzi (tutajadili hili siku zijazo). Uchaguzi mdogo wa ubunge Jimbo la Tarime pia unaweza kuthibitisha mtazamo wangu, kwamba chama kimoja cha upinzani kikijijengea uaminifu kwa umma na kufanya siasa za makini, si tu kinaweza kuishinda CCM bali kinaweza kuvishinda vyama vingine vingi.

Katika uchaguzi wa Tarime, CCM, Chadema, NCCR-Mageuzi na DP kila kimoja kilisimamisha mgombea wake, lakini ni chama cha upinzani cha Chadema ndicho kilichoweza kuibuka na ushindi na kuvishinda vyama vingine vyote, ikiwemo CCM.

Nguvu ya Chadema na kampeni makini iliyofanywa na chama hiki kule Tarime inaweza kuenezwa nchi nzima na chama hiki kikaweza kuing’oa CCM madarakani na hatimaye kuongoza nchi kwa kufuata sera zake ikiwa wananchi wataridhia hivyo.

Aidha, nguvu ya Chama cha NCCR- Mageuzi iliyoonyeshwa nchi nzima katika uchaguzi mkuu wa mwaka 1995, na nguvu ya CUF iliyoonyeshwa katika chaguzi zote tatu zilizopita, ule wa mwaka 1995, 2000 na mwaka 2005 kule kisiwani Zanzibar, zote zinathibitisha kuwa upo uwezekano mkubwa kwa CCM kung’olewa madarakani na chama kimoja cha upinzani iwapo kitajipanga na kuwa makini katika kufanya siasa zake.

Wajibu wetu kama wananchi ni kupima chama chenye muelekeo si tu wa kushinda katika uchaguzi lakini pia wa kutuongoza na kutufikisha kwenye ukombozi tunaouhitaji dhidi ya umaskini, ujinga, maradhi na umaskini.

Kuamini kuwa ili CCM ing’oke ni lazima wapinzani waungane ni kupotoka. Kutaka wapinzani waungane kwa lengo tu la kuing’oa CCM madarakani hakutatusaidia, ikiwa vyama vyenyewe vinapishana kisera na kiitikadi.

Tuendelee kutafakari na kuutafuta ukombozi wetu.

Waraka wa Kinabo: Hawa wanachelewesha ukombozi wetu

WATANZANIA wenzangu, wazalendo wa kweli wa Tanzania yetu, tutaweza kuing’oa CCM? Leo waraka wangu unajaribu kufanya tafakuri ya swali hili kwenu. Binafsi nalitafakari, nikiwa na sababu kuu mbili zinazonisukuma kufanya hivyo.

Kwanza, kama nilivyowahi kuandika awali, kuing’oa serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), iliyotawala nchi hii kwa zaidi ya miaka 47 (tangu TANU na ASP), ni muhimu mno katika kupisha mustakabali mpya wa ukombozi wa taifa letu dhidi ya umaskini, ujinga, maradhi na ufisadi. Katika hili nisisitize yafuatayo.

Ni muhimu CCM ing’oke kwani ndiyo chanzo na kikwazo kikuu cha matatizo yanayotukabili. Utawala wake wa muda mrefu, umekuwa wa kusuasua, wa kifisadi na usiokuwa na dhamira ya dhati ya kuwakomboa Watanzania.

Wingi wa raslimali na utajiri wa nchi yetu haviwiani na hali za maisha yetu, wala havilingani na umri wa uhuru wa nchi yetu, tangu tulipoupata mwaka 1961.

Kushindwa kwa CCM kumaliza au kupunguza umaskini wa nchi hii, kulibainishwa pia na hotuba ya bajeti mbadala ya kambi ya upinzani, iliyosomwa bungeni hivi karibuni na kiongozi wa kambi hiyo, Hamad Rashid Mohamed. Moja ya aya za hotuba hiyo, zilisema kama ifuatayo, ninanukuu:

‘‘Wakati CCM kinaendelea kupongezana kwa kunyosheana dole gumba, Watanzania wanaolala na njaa wameongezeka toka milioni 7.4 mwaka 1990 hadi kufikia milioni 14.4 mwaka 2007”, mwisho wa kunukuu.

Nikizingatia nukuu hiyo, ni muhimu CCM ing’oke ili tusitishe kasi hii ya ajabu ya kuongezeka kwa idadi ya maskini kila kukicha.

Ni muhimu CCM ing’oke kwani, kutokana na mfumo na kiwango cha kuchafuka kwake, hakuna tena uwezekano wa kutokea mtu atakayekuwa na uwezo wa kuleta mabadiliko kutoka ndani ya chama hicho.

Ni muhimu CCM ing’oke kwani wapo Watanzania wengi walio nje ya chama hicho, wenye uwezo wa kifikra na kiutendaji, wenye uchungu na nchi yao na wenye nia ya dhati ya kuikomboa nchi yao.

Pili, wakati ni muhimu kwa CCM kung’oka ili kupisha ukombozi mpya wa nchi hii, uzoefu wangu unaonyesha kuwa wapo watanzania wenzangu wenye mitazamo au imani zinazochangia sana kuchelewesha harakati za kuing’oa CCM kutoka madarakani.

Watanzania hao na mitazamo yao, naweza kuwagawanya katika makundi makuu matatu kama ifuatavyo;

Kundi la kwanza, ni lile la watu wasiojua, wasiojali au wasioamini kabisa kwamba siasa na uongozi wa serikali, vinaweza kufanikisha au kukwamisha jitihada za kutimiza ndoto za maisha yao.

Hili naliita kundi la kipekee. Naliita hivyo si kwa kulisifia bali ni kutokana na mtazamo wake wa kushtusha zaidi kulinganisha na makundi mengine nitakayoyajadili hapa chini. Kundi hili linaamini kuwa CCM ing’oke au ising’oke hilo si muhimu kwao.

Kwamba, itawale CCM, Cuf, CHADEMA, TLP, NCCR –Mageuzi au chama kingine chochote kile au kusiwe na serikali kabisa, wao hawajali, wanaona sawa tu.

Hawajali kwa sababu wanaona kufanikiwa, kukwama au kushindwa kwa maisha yao, hakuna uhusiano wowote na masuala ya kiserikali au utawala wa vyama vya siasa.

Hawa ndio wale ambao hawajiandikishi kupiga kura au wakijiandikisha hufanya hivyo kwa lengo la kupata vitambulisho tu lakini si kwa lengo la kutumia haki yao ya kuchagua chama au mgombea atakayeweza kuboresha maisha yao. Hawa pia ni wepesi sana kuuza shahada zao za kupigia kura pindi wanapofuatwa na viongozi au makada wa CCM.

Hawa wanaamini kuwa juhudi zao binafsi za kufanya biashara, kuchimba madini, sanaa, kuajiriwa, kulima na shughuli nyingine, zinatosha kabisa kutimiza ndoto za maisha yao.

Hawa hawapimi wala kujali athari chanya au hasi zitokanazo na maamuzi ya serikali. Baadhi yao wanapokwama kwenye shughuli za kutafuta mkate wao wa kila siku huamini wana nuksi, wamerogwa au Mungu hajapenda. Ni kawaida kuwasikia wenzetu hawa wakiizungumzia siasa kama ifuatavyo;

‘‘Jamani mie na hayo mambo ya siasa akaaa mwenzangu…siyawezi. Ashinde CCM, ashinde huyo CHADEMA, sijui na wale nani wengine wale, Cuf mie najionea yote sawa. Kwani huyo atakayeshinda ndiye atakayenipa ugali? Nikijiuzia vitumbua vyangu hapa nikapata unga wa kuwasongea ugali wanangu wakala, basi namshukuru Mungu. Hiyo siasa itanisaidia nini?

Hakika kundi hili lenye Watanzania wenye mtazamo huu, ndio kundi la kwanza na la msingi kabisa linalokwamisha au kuchelewesha kwa kiasi kikubwa harakati za ukombozi mpya wa nchi hii.

Kundi la pili, ni lile la watu wanaoamini kuwa CCM haistahili kung’oka na haitang’oka. Hawa wanaona CCM haistahili kung’oka kwa kuwa ni chama kizuri mno na kimeiongoza vema nchi hii katika kupata maendeleo na kudumisha amani, utulivu na umoja na mshikamano wa kitaifa. Kwa mantiki hiyo, wanaona kuwa ni halali CCM kuendelea kutawala.

Kwa watu hawa, hakuna chama chenye uwezo wa kuongoza nchi hii kama CCM kwani chama hicho ndicho kilichopigania uhuru wa nchi hii (tangu TANU na ASP). Hawa hupenda kusisitiza, ‘‘CCM ndiyo yenye uzoefu na nchi hii’’.

Wenzetu hawa wanaona CCM haiwezi kung’oka kwani licha ya kuiongoza vema nchi hii pia ni chama chenye nguvu mno, kinachokubalika kwa wanachi wengi. Hawaamini kama siku moja chama hiki kitang’oka. Wanaamini kitatawala milele na milele.

Hakika kundi hili la Watanzania wenye mtazamo huu nalo huchangia kwa kiasi kikubwa kuchelewesha ukombozi mpya wa taifa hili.

Kundi la tatu, ni lile la Watanzania wanaona kuwa CCM inastahili kung’oka kutoka serikalini, lakini hawaamini kuwa kama kuna chama au kutatokea chama kitakachokuwa na nguvu ya kuiong’oa CCM.

Kwa hawa, CCM inastahili kung’oka kwani hayo inayoyaita maendeleo ni kidogo mno kulinganisha na utajiri wa raslimali zilizopo katika nchi hii.

Wenzetu hawa hutumia werevu wao kulinganisha maendeleo yaliyofikiwa katika nchi nyingine zikiwemo zile tulizozitangulia kupata uhuru, mathalani Kenya, Botswana na Namibia na kugundua ni kwa kiasi gani CCM inavyowapotezea muda Watanzania.

Zaidi ya kutatizwa na ufukara uliokithiri, wenzetu hawa pia huona kuwa nchi yao imetawaliwa na matatizo mengi ya uonevu, unyonyaji, ubaguzi, upendeleo na ukandamizaji.

Kwa mantiki hiyo, shauku na sababu zao za kutaka CCM ing’oke zinafanana kabisa na sababu zile zile zilizowafanya mababu na mabibi zetu wapambane na wakoloni na hatimaye kufanikiwa kuwang’oa, wakiongozwa na Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.

Hawa wanaona kuwa amani na utulivu, umoja na mshikamano wa taifa vinavyodaiwa kudumishwa na CCM ni muhimu lakini si kila kitu kwa ustawi wa maisha yao, ikiwa chama hicho kimeshindwa kuondoa au kupunguza umaskini, ujinga, maradhi na ufisadi, vinavyowatafuna wao na nchi yao.

Hawa huona kuwa nchi yetu imechelewa mno, na inaweza ikapata maendeleo ya haraka mno (ikapaa), ikiwa serikali ya CCM itang’oka kupisha serikali ya chama kingine mbadala (wasichokijua), kuleta maendeleo kama yaliyofikiwa katika nchi jirani.

Lakini tatizo la watu wa kundi hili kama nilivyosema hapo juu ni kwamba, hawaamini kama CCM itang’oka. Kimsingi, wanatamani CCM ing’oke tena haraka iwezekanavyo, lakini hawaamini kama itang’oka, kwa sababu zifuatazo:

Kwamba, CCM haitang’oka kwa sababu ni chama chenye nguvu mno, chenye pesa nyingi, kikiwa na mtandao mkubwa wa viongozi na makada, kuanzia ngazi za chini kabisa za mashina, matawi, mabalozi wa nyumba kumikumi, uongozi wa vijiji, vitongoji, mitaa, kata, jimbo, wilaya, mkoa hadi taifa, wakifanya kazi ya kuvuna wanachama na kudumisha utawala wa chama hicho.

Kwamba, CCM haitang’oka kwa sababu ni chama kinachoshikilia serikali tangu mwaka 1961 kikiwa na sauti kwa tume ya uchaguzi (NEC), mahakama, majeshi, idara ya usalama wa taifa, na vyombo vyote vya ulinzi na usalama ambavyo huweza kuvitumia vibaya kudumisha utawala wake hata wanapotokea kushindwa kwa kura. Kwamba CHADEMA, Cuf au TLP, vikishinda nani atawatangaza kuwa washindi?

Kwamba, CCM haitang’oka kwa sababu vyama vya upinzani ni dhaifu, havina nguvu. Havina mtandao wa kutosha kutoka ngazi za chini hadi juu. Havina pesa, havifiki vijijini kwenye watanzania wengi.

Tena wapo wanaodiriki kusema (wengine wasomi), kwamba vyama vyote vya upinzani havina sera, vimetawaliwa na migogoro tu na viongozi wake wana uchu wa madaraka, ubinafsi na ukabila.

Hakika, kundi hili nalo la Watanzania wenye mtazamo huu, huchangia kwa kiasi kikubwa kuchelewesha harakati za ukombozi wa taifa hili, ingawa linautamani ukombozi huo. Ni kundi lililokata tamaa, ni Watanzania wanaoona giza nene mbele ya safari ya ukombozi wa nchi hii.

Kimsingi makundi mawili ya mwisho, lile la pili na la tatu, yanaamini kuwa CCM haiwezi kung’oka, tofauti zao ni kwamba kundi la kwanza linaamini CCM haistahili kung’oka wakati hili la pili linaamini kuwa inastahili kung’oka lakini haitang’oka.

Mitizamo na imani za watanzania wa makundi yote hayo vinakwamisha au kuchelewesha ukombozi mpya wa nchi hii, kwa sababu kwa ujumla wake, watu wa makundi yote hayo wana sababu au hoja zinazowafanya wasijue, wapotoke au wasiwe sehemu ya harakati za ukombozi wanaopaswa kuupigania na kuupata.

Hata hivyo, hoja na mitazamo ya makundi yote hayo kama nilivyofafanua, si za kupuuza. Kwa kiasi kikubwa hoja hizo, iwe ni kwa usahihi au upotofu wake, ndizo zinazochangia kuifanya CCM ionekane kuwa na nguvu kubwa kupindukia.

Kwa tafsiri ya mitazamo, imani na hoja hizo za baadhi ya Watanzania wenzetu (unaweza kuwa ni mmoja wao), ni kwamba tupende tusipende, CCM itatawala karne nyingi mno, itatawala milele na milele, itatawala daima.

Je, ni kweli CCM itatawala daima kama wenzetu hao wanavyoamini, tena wakiwa na hoja zao nzito nzito kama hizo? Je, tutaweza kuing’oa CCM inayopaswa kung’oka ili kupisha mustakabali mpya wa ukombozi wa taifa letu?

‘‘Watanzania wenzangu, kupitia waraka wangu kwenu, kwa kujiamini kabisa, natangaza unabii wangu juu ya mustakabali mpya wa uongozi taifa letu, kwamba Chama Cha Mapinduzi (CCM), kilichotawala nchi hii kwa zaidi ya miaka 47 sasa, toka enzi za TANU na ASP, kitang’oka kutoka kwenye serikali ya nchi hii.

…Niwe hai au mfu, nina hakika unabii huu mtakatifu na unaopaswa kutokea kwa manufaa ya vizazi vya leo na kesho vya taifa hili, utatimia.

Ndiyo, unabii huu utatimia kupisha zama mpya za utawala wa nchi hii, utawala utakaoleta haki palipo na dhuluma, upendo palipo na chuki na kuchochea maendeleo ya haraka na ya usawa kwa watu wote, yatakayosimika umoja na mshikamano wa kweli wa Watanzania wote”.

Kimsingi, kutokana na mfumo wetu wa kisiasa na kisheria, CCM kama chama cha siasa kinapaswa kung’olewa na chama kingine cha siasa. Kwa mantiki hiyo, tunapozungumzia harakati za kuing’oa CCM kutoka madarakani tunazungumzia harakati za kisiasa zinazofanywa au zinazoweza kufanywa na chama fulani cha siasa katika kuuvuta na kuunganisha umma wa Watanzania, kuelewa hasara za kutawaliwa na CCM na kuchukua wajibu wa kukipigia kura nyingi chama husika cha upinzani, kiingie serikalini. Katika hili kuna mambo yafuatayo yakutiliwa maanan.

Kwanza, ili kuiong’oa CCM kwa lengo la kuepukana na utawala wake usiofaa ni lazima kuwapo au kuanzishwe chama mbadala, ambacho kwa dira yake, maadili, miiko yake na dhamira yake kitaweza kuunda serikali mbadala itakayoondoa au kupunguza kwa kiasi kikubwa ubovu wa CCM isiyotakiwa.

Pasipo kuzingatia hili, kunaweza kukatokea hatari ya kuing’oa CCM iliyopo madarakani na kukiingiza chama kingine madarakani kisicho na tofauti yoyote na CCM.

Pili, ikiwa chama hicho mbadala kipo, basi pamoja na uzuri wake wa kiitikadi, kisera na dhamira yake ya kiutendaji, ni lazima chama hicho kiweze kufanya harakati madhubuti za kisiasa ili ndio kiweze kuungwa mkono na kuingia madarakani.

Itikadi, sera, kujua matatizo ya wananchi na kuwa na dhamira nzuri ya kuwaongoza vema wananchi, havitoshi kukifanya chama husika kiingie madarakani. Ni lazima chama hicho kifanye siasa ya kuwafikia, kuwaelewesha na kuwashawishi wananchi kukiunga mkono.

Tatu, katika kufanya siasa hiyo, ni muhimu kwa chama kinachotaka kuwa mbadala wa CCM kifahamu mitazamo ya Watanzania walio wengi juu ya siasa za nchi na hasa serikali ya chama kilicho madarakani. Kama tulivyoona hapo juu, si Watanzania wote walio maskini wanataka CCM ing’oke. Kwa mfano katika kundi la kwanza tuliona kuna Watanzania wenzetu ambao wamepigika kama sisi, wakifanya shughuli za ubangaizaji, tena wakikumbana na vikwazo kadhaa vya kiutawala.

Lakini bado wenzetu hawa uelewa wao haujafikia hatua ya kuuona utawala (serikali) kama ndiyo kikwazo chao kikuu. Huamini kuwa hawana bahati (nuksi), wamerogwa, mambo tu hayajaenda vizuri, si riziki au Mungu hajapenda.

Kwa mfano huo, ni muhimu kwa chama kinachotaka kuing’oa CCM kuielewa mitazamo kama hii ya wananchi wenzetu, ili kiweze kubuni mikakati madhubuti ya kuwaelimisha wananchi jinsi matatizo yao yanavyosababishwa na serikali, na jinsi matatizo hayo yanavyoweza kuondolewa kwa kuking’oa chama kilichounda serikali hiyo na kukiweka kingine madarakani.

Nne, ni lazima chama husika kibuni mkakati madhubuti wa kuwafikia na kuzungumza au kuwasiliana vema na wananchi, ili wajue uzuri wa chama hicho, vinginevyo bila kufanyika siasa hiyo, wananchi hawatajua dhamira na dira nzuri ya chama hicho katika kuwakomboa.

Tano, ni lazima chama kinachotaka kuwa mbadala wa CCM kielewe vema mfumo usio wa haki wa kisiasa, kama moja ya kikwazo kikuu dhidi ya harakati zake za kisiasa. Suala hili ni muhimu kwani linabeba zile hoja nzito za mtazamo wa Watanzania wa kundi la tatu, kwamba ni vigumu kuing’oa CCM kutoka madarakani kwa sababu tume ya uchaguzi ni yao, majeshi yote ni yao (yapo chini yao), mahakama zao na serikali pamoja na vyombo vyake vyote kwa ujumla, ipo chini yao.

Katika hilo la tano, uzoefu unaonyesha kuwa kuna hoja kuu mbili zinazokidhana. Hoja ya kwanza ni ile inayosema kuwa hakuna chama cha upinzani - hata kiwe kizuri vipi, kitakachoweza kuing’oa CCM hadi kwanza mfumo wa kisiasa utakaporekebishwa ili kujenga uwanja sawa wa ushindani kisiasa kwa vyama vyote.

Hoja ya pili inasema hivi, kwa kuwa chama kilicho madarakani (CCM), ndicho kilichouweka huo mfumo mbaya wa kisiasa ili kipendelewe na mfumo huo na kudumisha utawala wake, basi ni vigumu kwa chama hicho (kinachoshikilia makali), kukubali kuurekebisha mfumo huo, kwani kinajua fika kikifanya hivyo kitakuwa kinahatarisha nafasi yake ya kuwa madarakani.

Hoja hii inahitimisha kwa kusema hivi, njia muafaka lakini iliyo ngumu ni ile ya chama hicho mbadala kuamua kushindana na CCM ikitumia mfumo huu huu mbaya wa kisiasa kwani hakuna uwezekano wa CCM hiyo kukubali kuurekebisha.

Hoja hii ya pili pia inapinga mtazamo mwingine mwepesi unaovitaka vyama vya upinzani visusie uchaguzi hadi serikali ya CCM itakapokubali kurekebisha mfumo wa kisiasa kwa kuunda tume huru ya uchaguzi na kurekebisha sheria kadhaa za uchaguzi zinazokibeba chama hicho. Inahitimisha ikisema kuwa kususia chaguzi hakutaizuia CCM kuendelea kutawala, huku ikihalalisha utawala wake kauli mbalimbali za propaganda kama;

‘‘Wapinzani wameshindwa siasa, wamekubali tutawale baada ya kuona hawakubaliki”

Binafsi naungana na hoja hii ya pili, kwamba ni vigumu kwa serikali ya CCM kukubali kurekebisha mfumo wa kisiasa kwani uhai wa chama hicho unabebwa kwa kiasi kikubwa na mfumo huo. Kwa maneno mengine, tume huru ya uchaguzi itajenga uwezekano wa dhahiri wa chama hicho kushindwa uchaguzi kama hakitakubalika, kama vinavyoshindwa vyama vingine.

Uzoefu mdogo wa matukio ya kisiasa yaliyojiri nchi kwetu tangu kuanza kwa mfumo wa siasa za vyama vingi, unaashiria kuwa upo uwezekano wa CCM kung’olewa chini ya mfumo huu huu wa siasa tulionao. Nitoe mifano ifuatayo:

Chama cha Wananchi (CUF), karibu katika chaguzi zote, kimeweza kushinda viti vyote vya ubunge na uwakilishi kule kisiwani Pemba. Cuf imekuwa ikishinda katika mfumo huu huu wa kisiasa unaoibeba sana CCM, na si kweli kwamba CCM imekuwa ikiwaachia Cuf kushinda kisiwa chote cha Pemba. Wamekuwa wakikitamani sana lakini huzidiwa na kushindwa.

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), nacho kimeweza kushinda viti vingi sana vya udiwani katika uchaguzi mkuu uliopita wa mwaka 2005. CHADEMA hivi sasa ina madiwani takribani 102 nchi nzima. Hawa walipatikana wakati tume yetu sio huru na wala haitendi haki vya kutosha.

Aidha, chama hiki kiliweza pia kushinda chaguzi za ubunge mwaka 2005, kule Tarime, Mpanda Kati, Kigoma Kaskazini, Moshi Mjini na Karatu. Kutokana na ushindi wake huo, CHADEMA kikapata nafasi ya kuongoza serikali za halmashauri ya Karatu, Tarime na Kigoma ujiji. Hapa pia ni vema ikazingitiwa kuwa ushindi wote huu na mafanikio yote haya, yalipatikana katika uchaguzi ambao ulisimamiwa na tume isiyo huru tena ikisimamia sheria kadhaa za uchaguzi zinazoipa CCM mwanya wa kujifanya washindi. Huko kote, CCM walijaribu kufanya mbinu za kuungwa mkono walishindwa, walijaribu pia kufanya hia za kupoka ushindi nazo zilishindwa.

Kutokana na mifano hiyo, tunapata funzo kuwa Watanzania tunaweza kabisa kuishinda na kuing’oa CCM hata kama majeshi ni yao, tume ya uchaguzi yao, na mahakama ziko chini ya serikali ya chama hicho. Msingi wa uwezo wetu huo unajikita katika falsafa ya nguvu umma kuwa kubwa zaidi kuliko nguvu ya utawala (serikali) na vyombo vyake.

Hii inatuashiria kuwa iwapo umma wa Watanzania wa maeneo yote utaelimishwa kisiasa juu ya ubaya wa CCM na kuhamasishwa kuchukua wajibu wa kuing’oa bila uwoga kama ilivyofanyika kule Pemba, Tarime, Karatu, Moshi Mjini, Mpanda Kati, Kigoma Kaskazini na Kigoma Ujiji, basi Tanzania yetu itaweza kabisa kujikomboa kutoka kwenye utawala dhalimu wa CCM.

Tunaweza kupata rais na wabunge wengi kutoka chama mbadala cha upinzani, ikiwa tu umma wote utaelemishwa vema, kuhamsishwa na kutiwa ujasiri wa kutosha kama ilivyofanyika katika maeneo hayo niliyoyatolea mfano.

Nguvu ya umma wenye ujasiri wa kutosha inaweza kabisa kuwafanya vijana wetu walio kwenye majeshi kutothubutu kuipendelea CCM. Vijana walio kwenye vyombo vya ulinzi na usalama vinavyoibeba CCM leo hii, wanaweza kabisa kuchotwa na mwamko wa nguvu ya umma wa Watanzania walio wengi na kujikuta wakiiasi CCM na kutenda haki, ili kuepuka kumwaga damu za Watanzania wenzao. Hali kama hiyo au inayofanana na hiyo ndiyo iliyotokea katika maeneo kadhaa ambayo vyama vya upinzani vimeweza kushinda.

Kumbe inawezekana kabisa kwa CCM kung’olewa kutoka madarakani katika mazingira haya haya tuliyonayo!. Kinachotakiwa ni uwepo wa chama mbadala kinachoweza kuwaelimisha, kuwaunganisha, kuwahamasisha na kuwatia ujasiri Watanzania walio wengi katika kuikataa na kuing’oa CCM.

Aya za Ukombozi: Kutoka uchaga hadi ukatoliki, tuwaeleweje?

WIKI chache kabla ya kuanza rasmi kwa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa rais, wabunge na madiwani, nawasilisha aya hizi kuvikumbusha vyombo vya habari kuwa havipaswi kufungamana na chama wala wagombea, lakini wakati huo huo kila chombo cha habari kina haki na wajibu wa kupinga na kulaani jitihada zozote za makusudi zinazofanywa na watu au chombo kingine cha habari, zenye lengo la kuchonganisha, kuchochea au kupandikiza chuki na ubaguzi wa aina yoyote ile dhidi ya Mtanzania yeyote yule, iwe ni dhidi ya mwanasiasa au mwananchi wa kawaida.

Nikiitumia safu ya ‘Waraka wa Kinabo’, nimewahi kukemea na kulaani uchochezi na ubaguzi wa kidini na kikabila kuwa ni hatari kwa umoja na mshikamano wa taifa na hatari kwa amani na maendeleo yetu lakini hali hiyo imekuwa ikiendelezwa kwa makusudi.

Leo nimelazimika tena kuurudia wajibu wangu huo, baada ya kuona siasa hizo chafu zikitamalaki kwa kasi kubwa kutoka kwa wanasiasa ucharwa hadi kufikia kubebwa na baadhi ya vyombo vya habari vilivyojipatia heshima kubwa miaka ya nyuma kwa kuelimisha jamii na sasa kuonekana kubadilika na kutoa baadhi ya habari zinazoonekana dhahiri kuipotosha jamii.

Ndani ya kipindi cha takriban wiki mbili sasa tangu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Dk. Willbrod Slaa, akubali na kutangazwa kugombea urais kupitia chama hicho, kumekuwa na habari zinazoonekana dhahiri kuandikwa kimkakati (propaganda) zikilenga kuushawishi umma umbague mwanasiasa huyo kwa sababu ya dini na dhehebu lake.

Mfano mkubwa wa habari hizo ni ile iliyoandikwa na gazeti moja wiki iliyopita ikitaarifu kuwa wabunge Waislamu wa CHADEMA waliamua kususia mikutano ya Dk. Slaa anayoifanya kutafuta udhamini maeneo mbalimbali nchini kwa madai ya kuchukizwa na mgombea huyo kutumwa na maaskofu kugombea urais.

Tukiitazama kwa umakini habari hiyo tutabaini kuwa gazeti husika liliamua kwa makusudi kuwaandika wabunge hao wa CHADEMA kwa kutazama na kutumia zaidi kigezo cha dini zao (Waislamu) kuliko sababu za msingi zilizowafanya wakosekane kwenye mikutano hiyo.

Izingatiwe kuwa mmoja wa wabunge ambaye hakuwepo, Zitto Kabwe, alihojiwa na kukijibu chombo hicho kwamba kutokuwepo kwao kwenye mikutano hiyo kulisababishwa na wao kuwa na ratiba majimboni mwao lakini katika kile kinachoonekana ni kulazimisha na kukoleza chuki na ubaguzi wa kidini dhidi ya Dk. Slaa, chombo hicho kiliichapa habari hiyo huku kichwa cha habari na maudhui yake vikionekana dhahiri kuupa nafasi kubwa na kuupambanisha kwa makusudi Uislamu wa wabunge hao dhidi ya Ukiristu wa Dk. Slaa bila sababu za msingi.

Pasipo shaka yoyote ile, nathubutu kuthibitisha kuwa huu ni uchochezi unaopaswa kuchukuliwa hatua na mamlaka husika, si kwa kusubiria hadi aliyeguswa alalamike kwa Waziri wa habari au Baraza la Habari, bali kwa mamlaka husika kuwajibika mara moja na kuchukua hatua stahiki dhidi ya chombo husika, kwani athari ya uchochezi huo haiishii kwa Dk.Slaa na chama chake tu bali pia kitendo hicho kwa taathira yake ni hatari kwa taifa zima.

Kinachoshangaza na pengine kusikitisha zaidi ni suala hilo kuendelea kukuzwa na kulazimishwa kwa staili hiyo licha ya ukweli kuwa tayari Kanisa Katoliki lenyewe lilishakanusha rasmi madai ya kumtuma Dk. Slaa kugombea urais tangu ilipochapwa gazetini habari iliyotangulia, iliyokuwa na maudhui yanayofanana kidogo na habari hii iliyofuatia.

Uandishi wa aina hiyo unaonekana dhahiri kuwa na lengo la kuwapotosha na kuwagawa Watanzania wapige kura kidini pengine kwa matakwa na masilahi ya chama au mgombea wa urais anayeungwa mkono na chombo husika cha habari.

Hali hii inaweza kusababisha Watanzania wasio waangalifu kupumbazwa na habari hizo na kujikuta wakiacha kumchagua mgombea anayestahili na matokeo yake taifa kujikuta likipata viongozi wabovu waliochaguliwa kwa sababu ya dini au makabila yao badala ya sifa za uwezo wao wa kiuongozi. Kwa mantiki hiyo, nathubutu kusema tena hapa kwamba, habari ya namna hiyo hazina maslahi kwa taifa kwani kwa taathira yake zinaweza kuhujumu haki na utashi wa Watanzania kuchagua kiongozi atakayewafaa.

Aidha, nikumbushe kwamba si mara ya kwanza kwa gazeti hilo au mengineyo yenye muelekeo kama huo kuandika habari zenye kuhamsha hisia za ubaguzi kwa mtindo wa kuonyesha madai ya kuwepo ubaguzi. Katika kile kinachoonekana kuwa ni mkakati, mara zote hizo, CHADEMA ndiyo imekuwa mhanga mkuu wa habari hizo.

Mathalani, wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005, waliandika kile walichokiita kuwa ni ukabila ndani ya CHADEMA, wakijaribu kuushawishi umma ukione kile kilichodaiwa kuwa ni upendeleo wa Wachaga (Uchaga) ndani ya chama hicho. Hilo likarudiwarudiwa mara kadhaa na kukuzwa zaidi hata baada ya uchaguzi ule.

Ilipokosa nguvu wakaandika madai kuwa CHADEMA ni chama cha watu wa Mkoa wa Kilimanjaro. Mkurugenzi wa Mambo ya Nchi za Nje wa chama hicho, John Mnyika, ambaye kabila lake ni Msukuma naye wakamchokonoa na kubaini kuwa mama yake ni Mpare na kutumia kabila hilo la mama yake kuhalalisha madai yao dhaifu kwamba CHADEMA ni chama cha watu wa Kilimanjaro. Vituko vitupu!

Madai ya chama cha Kilimanjaro yalipochuja yakaongezewa nguvu mpya, sasa chama hiki kikadaiwa kuwa ni chama cha upendeleo kwa watu wa ukanda wa kaskazini. Yote matatu, ‘Uchaga’, ‘Kilimanjaro’ na “Kanda ya kaskazini” yakarudiwarudiwa kwa miaka minne mfululizo yakishereheshwa na hoja dhaifu zilizoonekana kuupima au kuuchezea uwezo wa kufikiri wa Watanzania lakini wapi – propaganda hizo zilikosa mvuto. Madai yote yakakosa mashiko.

Chama kilichodaiwa cha Wachaga, cha Kilimanjaro, cha Kaskazini, juzi kilikuwa Musoma na Mwanza, jana kilikuwa Shinyanga na Kagera, kinafanya nini kote huko?

Mara zote uchambuzi makini ungeweza kujiridhisha pasipo shaka yoyote ile kuwa, habari hizo zilikuwa zikilenga tu kukiondolea imani chama hicho au viongozi wake ndani ya mioyo na fikra za Watanzania. Kinyume chake walengwa wa propaganda zote hizo (CHADEMA na uongozi wake) wameendelea kuimarika na kuonekana kuungwa mkono na Watanzania wa kada zote, wakiwemo wasio na dini, wenye dini na makabila yote. Sasa umeibuliwa wimbo mpya ‘udini na ukatoliki’, hii ndiyo santuri mpya nayo kama zilivyokuwa santuri zilizopita inaonekana kukosa mashabiki. Tusubiri tuone.

Kutoka Uchaga hadi Ukatoliki; tuwaeleweje watu hawa, tuvieleweje vyombo hivi vya habari, tuwaeleweje wanasiasa hawa? Jibu la msingi ni moja tu, nalo ni lile lililowahi kutolewa na Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere, kwamba “wamefilisika kisiasa”.

Upande wanaoupigania umepwaya, hauna hoja za msingi za kujihalalisha kwa umma, ndiyo maana zinafanyika jitihada nyingine za pembeni zikijaribu kutumia ukabila na udini kuwatafutia uhalali mpya watawala walioshindwa kuthibitisha uhalali wao wakiwa madarakani.

Wanajua fika kwamba sekondari za kata si kigezo cha kumhalalisha mgombea wao mbele ya umma wa Watanzania waliojipatia elimu na maarifa kupitia shida za nchi yao licha ya kunyimwa elimu bora na serikali yao.

Wanajua fika kwamba vigogo wachache waliofikishwa mahakamani kwa tuhuma za rushwa na matumizi mabaya ya madaraka sio kigezo cha msingi cha kumhalalisha mgombea wao aliyeshindwa kutumia vizuri madaraka yake kunusuru fedha na raslimali nyingi za umma.

Wanajua fika kwamba wasifu na uwezo wa mgombea wao hautoshi kumhalalisha mbele ya umma wa Watanzania utakapolinganishwa na wasifu na uwezo wa Dk.Slaa aliyevuta hisia za Watanzania wengi ndani ya wiki mbili tu tangu alipokubali kuwania wadhifa huu mkubwa.

Wana hofu ya msingi kuwa Dk. Slaa aliyefanya kazi kubwa jimboni, bungeni na nje ya Bunge kwa miaka kumi na tano sasa, amejipatia umaarufu, umashuhuri na uhalali mkubwa wa kupewa dhamana ya kuliongoza taifa kuliko yule aliyepewa dhamana hiyo lakini akalirudisha nyuma.

Wanajua fika kuwa hata jina la ‘Dokta’ linalotumiwa na mgombea wao ni la kupewa kwa heshima tu na wala halijatokana na kufikia ngazi ya elimu ya udaktari wa falsafa “PHD” aliyonayo Dk. Slaa. Kwa mantiki hiyo wanajua fika kuwa hawana miujiza hata ile ya kumtengenezea sifa za ziada mgombea wao na chama chao, sasa wamebakiwa na mkakati mmoja tu, nao ni kujaribu kuharibu sifa za Dk. Slaa kwa kuihusisha hatua yake ya kuwania urais na ukatoliki na historia yake ya kuwa padri, ili kuibua hisia za ubaguzi miongoni mwa Watanzania dhidi ya mwanasiasa huyo. Tukikubali kuingia kwenye mtego wa kutufanya anayetufaa tumuone hatufai, basi tutakuwa tumekubali kukwamisha harakati za kuufikia ukombozi mpya wa taifa letu. Tusikubali.

Wana falsafa wana msemo usemao: “Ni mjinga yule asiyesoma, lakini ni mjinga zaidi yule anayeamini kila kitu anachokisoma”. Tusome magazeti lakini tusiamini kila kitu tunachokisoma, yapo yanayokosewa kwa bahati mbaya na wakati mwingine yapo yanayoandikwa kwa makusudi kupotosha au kutimiza malengo fulani yasiyo na maslahi kwetu sisi kama wananchi.

Ni wajibu wa kila mmoja wetu kuvichunguza na kuvifahamu vyombo vyote vya habari vinavyoandika na kuripoti habari za aina hiyo na hatimaye kuvipuuza na kuviacha vikijifia vyenyewe kwa ama kukosa soko au kukosa wasomaji kwa sababu ya habari hizo ambazo nathibitisha pasipo shaka yoyote ile kwamba hazilitendei haki wala kulitakia mema taifa hili.

Kwa aya hizi, nauenzi na kuueneza wasifu wa Baba wa Taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere, kwamba: “Hatutamkataa mtu kwa sababu ya kabila lake lakini hatutamchagua mtu kwa sababu ya kabila lake.” Vivyo hivyo, “haitatusaidia kumkataa mtu kwa sababu ya dini yake wala kumchagua mtu kwa sababu ya dini yake”. Tuweke mbele masilahi ya taifa letu.